Ukosefu wa ajira huwakatisha watu tamaa na hata kuwafanya washawishike kujiunga kwenye vitendo visivyofaa, maana hapo kabla walikuwa wakiamini baada ya masomo kupata kazi ni mteremko Msongo wa mawazo au kukata tamaa, haviwezi kukusaidia kukuondoa kwenye hali uliyonayo.
Huna ajira hilo ni sawa lakini unapaswa kutambua kuwa hiyo hali ni ya kupita. Baki na matumaini kuwa utapata kazi nzuri kulingana na vigezo vyako vya kitaaluma na ujuzi mzuri ulionao. Endelea kujiamini kuwa wewe ni mtu bora kikazi ambaye muda ukifika utauonyesha na kutoa kila ulichonacho.
Kuna kanuni tatu ambazo unapaswa kuzizingatia unapokuwa kwenye changamoto ya kukosa ajira, kwanza ni kujijali. Jipende na ujijali kila wakati. Usiyafanye macho ya pembeni yakuone unadhoofika au unakuwa mchafu, kisa huna kazi!
Vaa vizuri na uonekane nadhifu, kwani usafi wako unaweza kumvutia mtoa ajira.
Kanuni ya pili ni kutabasamu. Usishike tama, onekana na tabasamu lako kila wakati. Ukitabasamu mbele za watu na wenyewe watatabasamu.
Kanuni ya tatu na mwisho ni kuchangamka. Ukikutana na watu changamka na uonyeshe upo vizuri kiakili na kimwili. Uchangamfu wako hutoa picha kwamba afya yako ya mwili na akili vipo imara. Baada ya hapo zingatia mambo matano yafuatayo.
Jiweke sokoni
Andaa wasifu wako (CV) ambayo umeuandika vizuri kisha uwasilishe kwenye maeneo unayoona yanafaa au yale ambayo ungependa upate kazi. Usikae tu kwa sababu umeambiwa ajira hakuna. Hapana, jiweke sokoni ujulikane.
Kimsingi, unatakiwa urahisishe upatikanaji wako. Simu yako iwe wazi ili ukipigiwa upatikane. Wengi hukosa ajira kwa sababu ya kuweka namba za simu zisizo na uhakika, anapigiwa hapatikani. Wenye kutafuta ajira ni wengi, aliye rahisi kupatikana ndiye hupewa kipaumbele.

Jiongezee thamani
Kipindi ambacho huna ajira, unaweza kukitumia kujiongezea thamani kwa kusoma kozi tofauti zenye kuongeza uzito wa ujuzi au taaluma uliyonayo. Lazima ufahamu kuwa wanaoshinda kwa urahisi katika soko la ajira ni wale wenye sifa za ziada.
Tumia muda wako kusoma lugha za kimataifa. Siku ukiingia kwenye mchakato wa ajira, utajikuta ni bora zaidi kwa sababu unaweza kuzungumza na kuandika kwa kutumia lugha nyingi kuliko wenzako.
Jiongeze thamani kwa kusoma zaidi kompyuta. Ulimwengu wa teknolojia huu; fikiria unaomba kazi ya uofisa mauzo, pamoja na kuwa na sifa zinazotosha kupata kazi hiyo, unakuwa na nyongeza ya kujua kompyuta kwa sababu ulisoma pia Tehama.
Nenda chuo cha udereva na ukishafuzu fanya mchakato upate leseni. Thamani yako inaweza kuongezwa na hilo, kwamba wenzako walioomba watahitaji dereva kutimiza majukumu yao, wakati wewe unaweza kujiendesha mwenyewe kama utapewa gari na ofisi.
Jitangaze kisasa
Tambua ulimwengu uliopo kisha utumie urahisi wa kiteknolojia kujitangaza. Wewe ni mhandisi, hakikisha unafungua blogu na kuwa na akaunti za mitandao ya kijamii ambayo utaitumia kuandika na kutoa ushauri wa kitaalamu kuhusu eneo lako.
Utakapokuwa unaandika utawafanya watu wengi zaidi wakuone. Matokeo yake utaonwa na waajiri. Jinsi ambavyo unajipambanua kwa kueleza kasoro za kiutendaji katika eneo lako na kutoa mwanga wa kile ambacho kinapaswa kufanyika, itawafanya waajiri wakuone wewe ni bidhaa bora kuwa nayo.
Unaweza kujitangaza pia kwa kuomba kurasa kwenye magazeti. Kuliko kukaa tu bila kazi, hebu kile ambacho unacho kichwani kiweke kwenye maandishi kupitia magazeti. Omba kuhojiwa redioni na kwenye televisheni, huko ndiko kujitangaza kisasa.
Inawezekana waajiri hawasomi blog yako, hawapitii mitandao ya kijamii wakaona kile ambacho umekuwa ukikitoa lakini siyo tatizo. Andaa vipande vya video au maandiko yako na kupeleka kwa waajiri. Hapo unakuwa unajiweka katika hali inayoutangulia wakati uliopo.
Jitolee kufanya kazi
Omba kazi ya kujitolea ukiwa unajiamini kuwa baada ya muda wewe ni rasilimali inayohitajika. Unapokuwa unajitolea hakikisha unatoa kila ulichonacho ili kuwapa hamu waajiri waone ulazima wa kukaa na wewe mezani na kujadiliana jinsi ya kufanya kazi pamoja kwa mkataba wa muda mrefu.
Unaweza kujitolea pia kwa kufundisha. Unapokuwa unaingia darasani kufundisha inakusaidia kuendelea kutunza kile ulichonacho na kujiogezea. Kimsingi, kufanya kazi kwa kujitolea kuna maana kubwa na kunakufanya uwepo kwenye mzunguko wa ajira.
Iwe kujitolea kufanya kazi mahali au kwa kufundisha, muhimu ni kuwa inakuongezea thamani kwenye CV yako. Inakupa ile hadhi ya uzoefu ambayo hutakiwa na waajiri wengi.
Watu ambao wametoka chuo na hawajawahi kufanya kazi hiyo mahali popote huogopwa na waajiri, kwa maana huonekana huingia kazini kama wanafunzi wenye kuhitaji maelekezo na mafunzo mengi ili waijue kazi.
Unaweza kujiajiri
Usikae tu damu yako italala, wakati ambao upo na ari ya kufanya kazi lakini ajira hakuna, hebu angalia jinsi ya kujitengenezea ajira. Umesomea masuala ya uongozi wa biashara, unaweza kujiajiri kama mshauri wa usimamizi wa biashara.
Angalia ulichosomea, kisha kitengenezee ajira binafsi au hata kuajiri wengine. Siy vibaya ukajiajiri kwenye mambo mengine ambayo hata hukusomea, ilimradi unaona urahisi kuanza na kufanikiwa. Usibweteke kwa kukosa ajira, amka na uonyeshe matokeo.
JIUNGE NASI KWA KUTUFOLLOW
fb@edonetz  , twiter@edonetz  , inst@edonetz_blog  na  youtube@edone tv
 
Top