Tuanzie huko Kisangani ,Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo
Wapinzani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wamekusanyika katika mji wa Kisangani nchini humo wakitaka kuachiwa huru wanaharakati wa kisiasa wanaoipinga serikali. Benjamin Ntumba mmoja
wa wanaharakati wa chama cha Upinzani cha  Umoja kwa ajili ya Demokrasia na Maendeleo ya Jamii (UDPS) amesema kuwa wapinzani Kongo  wamekusanyika katika mji wa Kisangani kulalamikia hatua ya Mahakama moja mjini humo ya kukataa kuwaachia huru wapinzani sita wa kisiasa.
Benjamin Ntumba mwanaharakati wa chama cha upinzani Kongo cha (UDPS)
Wanaharakati hao sita wa kisiasa wanaoipinga serikali ya Kinshasa wanashikiliwa mahabusu huko Kisangani tangu tarehe 19 mwezi uliopita hadi sasa. Benjamin Ntumba ameashiria  kuachiwa huru watu wengine ambao walitiwa mbaroni pamoja na wanaharakati hao sita na kusisitiza kuwa, wanaharakati hao wa kisiasa wanaoipinga serikali ya Kongo wamekatwa kinyume cha sheria. Ntumba ametaka wanaharakati hao waachiwe huru haraka na bila ya masharti yoyote.
Na tukielekea huko Africa kusini ni kwamba..
Maandamano ya wanachuo nchini Afrika Kusini yanaripotiwa kuongezeka baada ya baadhi ya vyuo kufunguliwa.
Mamia ya wanachuo wa Chuo Kikuu cha Wits cha mjini Johannesburg leo wameandamana wakilalamikia sera za serikali katika kushughulia hali ya wanachuo.
Taarifa zaidi zinasema kuwa, barabara za Chuo Kikuu cha Wits leo zimeshuhudia maandamano makubwa ambayo yameingiliwa kati na polisi na kupelekea kutokea vurugu kubwa.
Vitendo vya vyombo vya usalama vya Afrika Kusini vya kutumia mabavu dhidi ya maandamano ya amani ya wanachuo hao vinakithiri katika hali ambayo, masomo katika vituo vingi vya elimu na Vyuo Vikuu yamesimamishwa  katika mji wa Johannesburg.
Wanafunzi wa vyuo vikuu nchini Afrika Kusini wamekuwa wakifanya maandamano ya amani kwa muda sasa kulalamikia siasa za serikali ya Rais Jacob Zuma na mazingira yao ya masomo.
Kilio kikubwa cha wanachuo hao ni ongezeko kubwa la karo na takwa lao la kuongezewa posho.
Hata hivyo maandamano hayo ya amani ya wanachuo yamekuwa yakizusha vurugo na fujo kati yao na vyombo vya usalama ambavyo vimekuwa vikitumia mabomu ya machozi na risasi za blastiki kuwatawanya wanachuo hao.
Mara kadhaa kumefanyika mazungumzo ya wakuu wa vyuo vikuu vya Afrika Kusini na wawakilishi wa vyama vya wanachuo lakini mazungumzo hayo yameshindwa kuzaa matunda.

Na huko  Israel
Afisa wa ngazi za juu wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS amesema kuwa, harakati hiyo itatoa jibu kali kwa shambulio lolote tarajiwa kutoka kwa utawala haramu wa Israel.
Dakta Mahmoud al-Zahar ametangaza kuwa, Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS itajibu kwa nguvu zake zote jinai yoyote ile itakayofanywa na utawala ghasibu wa Isarael dhidi ya wananchi wa Palestina.
Kiongozi huyo wa ngazi za juu wa Chama cha Hamas ameashiria vitisho vya utawala haramu wa Israel dhidi ya Ukanda wa Gaza na kusema kuwa, endapo utawala huo ghasibu unataka kuanzisha vita vipya katika eneo, basi mapambano na muqawama wa wananchi wa Palestina umejiandaa kukabiliana vilivyo na uchokozi huo.
Amesema, mahesabu ya Avigdor Lieberman, Waziri wa Vita wa utawala haramu wa Israel ya kutaka kuishambulia Gaza ni propaganda zenye lengo la kutoa pigo kwa eneo hilo na kuongeza kuwa, waziri huyo wa Kizayuni anataka kuzionesha fikra za waliowengi katika jamii ya Wazayuni kwamba, utawala huo umetoa pigo kwa muqawama na mapambano ya wananchi wa Palestina.
Mahmoud al-Zahar ameeleza kuwa, machafuko na vita vyovyote vile katika mipaka ya Gaza na ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu vitapelekea maelfu ya walowezi wa Kizayuni kukimbia na ni kwa msingi huo, viongozi wa Israel hawawezi kuanzisha vita vingine.
Tumalizie na huko niger
Ofisi ya Rais wa Niger imetangaza siku mbili za maombolezo nchini humo baada ya mauaji ya wanajeshi kadhaa katika shambulizi lililofanywa dhidi ya kambi ya wakimbizi wa Mali huko kaskazini mwa Niger.
Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Rais wa Niger imesema kuwa, nchi nzima itakuwa katika maombolezo ya taifa kwa muda wa siku mbili baada ya mauaji ya wanajeshi 22 katika shambulizi lililofanywa na kundi moja la watu waliokuwa na silaha dhidi ya kambi ya wakimbizi wa Mali katika eneo la Tazalit.
Wizara ya Ulinzi ya Niger imetangaza kuwa, askari 14 wa Gadi ya Rais, polisi 5 na wanajeshi 3 wa nchi hiyo wameuawa katika shambulizi hilo na wengine watatu wamejeruhiwa. Msemaji wa Wizara ya Ulinzi ya Niger, Moustapha Ledru amesema kuwa, kundi lililofanya mauaji hayo limekimbilia katika ardhi ya nchi jirani ya Mali na kwamba, operesheni ya kuwasaka inaendelea. Maafisa usalama wa Niger wanasema, shambulizi hilo limefanywa na kundi la kati ya watu 30 hadi 40 ambao walikuwa wakizungumza lugha ya watu wa kabila la Tuareg.
Wakati huo huo Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika Bi Nkosazana Dlamini Zuma amelaani shambulizi hilo na kutoa salamu za rambirambi kwa serikali ya Niger na familia za wanajeshi hao. Dlamini Zuma ametangaza tena upinzani wa Umoja wa Afrika dhidi ya ukatili, ugaidi na misimamo mikali na kusema: AU itaendeleza jitihada za kushirikiana zaidi na serikali ya Niger, nchi za eneo la Ziwa Chad na jumuiya za kimataifa kwa ajili ya kupambana na ugaidi na misimamo mikali inayoua maelfu ya watu wasio na hatia na kuwalazimisha mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi.
Katika upande mwingine Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amesisitiza udharura wa kuchukuliwa hatua kali zaidi za usalama nchini Niger. Ban Ki-moon ameitaka serikali ya Niamey kuzidisha ulinzi kwenye kambi ya wakimbizi wa Mali kwa ajili ya kulinda usalama wao. 
Kwa sasa jeshi la Niger limeanzisha operesheni kubwa ya anga na nchi kavu kwa ajili ya kuwasaka wanachama wa kundi lililofanya mauaji ya wanajeshi hao ingawa hadi sasa operesheni hiyo haijafanikiwa. Makundi kadhaa ya kigaidi yenye mfungamano na kundi la al Qaida yamejikita katika eneo la kaskazini mwa Mali tangu miaka mitano iliyopita na yamekuwa yakifanya mashambulizi na mauaji ya kutisha katika eneo hilo na kwenye mpaka wa Mali na Niger. Shambulizi la sasa dhidi ya askari wa Niger limefanyika baada ya serikali ya Niamey kurefusha kipindi cha hali ya hatari katika maeneo ya kusini mashariki mwa nchi hiyo. Serikali ya Niger imetangaza kuwa, sababu ya kurefusha hali hiyo ni mashambulizi yanayoendelea kufanywa na wanachama wa kundi la kigaidi la Boko Haram. 
Katika mazingira haya inaonekana kuwa, shambulizi lililofanywa na kundi la watu wasiojulikana dhidi ya wanajeshi wa Niger ni tishio jingine kubwa kwa usalama wa nchi hiyo.
Kwa muda sasa nchi za eneo la Ziwa Chad zimeanzisha mashambulizi ya kupambana na kundi la Boko Haram na makundi mengine ya waasi lakini operesheni hiyo haijapata mafanikio ya kuridhisha. Hii ni pamoja na kuwa, kuendelea kwa wimbi la wakimbizi wanaohama kutoka maeneo ya vita na kwenda maeneo salama katika nchi jirani kama Niger ni tatizo jingine linalozitatizo nchi hizo. 

Shambulizi la kigaidi la siku kadhaa zilizopita nchini Niger ni kengele nyingine ya hatari kubwa ya harakari za kigaidi za makundi ya waasi katika eneo hilo la magharibi mwa Afrika. Kwa msingi huo inaonekana kuwa, kuna haja ya kuimarisha vikosi vya jeshi katika maeneo ya mpakani na kushirikiana zaidi kwa ajili ya kung'oa mizizi ya makundi hayo kupitia ratiba na mpango maalumu.         
 
Top