Katika  elimu mpya kabisa ya uzazi ambapo mwanamke yeyote anaweza kupata ujauzito wenye watoto mapacha hata kama si asili ya ukoo wake. Tunaweza kusema  mwanamke yeyote  kwa sababu kuna imani ya miaka na miaka kwamba, si kila mwanamke anaweza kupata ujauzito bali itategemea na asili yake. Na kuna  Baadhi ya mila na desturi, hasa katika nchi za Kiafrika zinaamini kwamba, mwanamke kupata watoto mapacha kunatokana na urithi wa kizazi chake, kuanzia mababu wa upande mmoja kati ya wanandoa hivyo uzao huo hufuata mkondo kwa miaka na miaka. Wengi wakipata mapacha huulizwa kama kwenye kizazi chake, kuna watoto mapacha. Akitokea mama akasema hakuna, basi huaminika kwamba lazima upande wa mwanaume kuna waliowahi kuzaliwa mapacha  
kwa mfano: Mwanamke ambaye mke wa mjomba wake ana mapacha haimpi yeye nafasi ya kupata mapacha kwa sababu hana uhusiano na mke wa mjomba wake kibailojia. Ila mwanamke ambaye dada yake ana mapacha inampa uwezekano wa kupata watoto mapacha kwasababu wana uhusiano wa moja kwa moja.
Hembu tujifunze hatua moja baada ya nyingine. Na kisha tuone jinsi gani mimba ya watoto mapacha inavyotungwa.
Kwanza tujue Mimba inatungwaje?
Kipindi cha ovulation ndipo ambapo mwanamke anaweza kushika mimba. Ovulation ni kipindi ambacho yai kubwa ama yai lililo tayari hutoka kuelekea kwenye tumbo la uzazi kupitia mirija ya ovari. Yai hilo kwa bahati nzuri likikutana na mbegu ya kiume hurutubishwa katika kipindi cha masaa 24 (baada ya muda huo yai hupoteza uwezo wake). Iwapo yai litarutubishwa ndani ya muda huo na kisha kujikita katika mfuko wa uzazi basi mimba itakuwa imetungwa. Iwapo yai halikurutubishwa hutolewa nje kama damu ya hedhi.
Na sasa tuangalie Mapacha hutokeaje?
Hapa tukumbuke kuwa kuna mapacha wa aina mbili: Mapacha wanaofanana (Identical twins) na Mapacha wasiofanana (Fraternal twins). Mapacha wasiofanana hutokea pale mwanamke anapotoa mayai mawili kuelekea kwenye tumbo la uzazi. Hii ina maana ni mwanamke ama mwili wa mwanamke unaosababisha mayai mawili kuachiliwa kwa pamoja. Baada ya hapo mayai haya hukutana na mbegu za kiume ambapo hurutubishwa ndani ya muda maalumu na kisha hujikita kwenye mfuko wa uzazi. Hivyo basi hata kama mwanaume angetoa mbegu milioni moja lakini yai la mwanamke likitoka moja basi mtoto atakayepatikana atakuwa ni mmoja tu.
Huo ni upande wa mapacha wasiofanana (Fraternal twins). Kwa upande wa mapacha wanaofanana (Identical twins) hadithi ni tofauti kidogo. Baada ya yai kurutubishwa na mbegu ya kiume na kujikita kwenye mfuko wa uzazi kwa sababu zisizofahamika kisayansi huamua kujigawa na kutengeneza watoto mapacha. Mapacha hawa kwa kawaida hufanana sana na huwa ni wa jinsia moja tofauti na fraternal twins ambao huweza kuwa wa jinsia mbili tofauti ama jinsia moja.
Kutokana na maelezo hayo hapo juu inaonyesha kwamba watoto mapacha wanaofanana ama wasiofanana husababisha na mwanamke ambaye kwa sababu moja ama nyingine mwili wake huachilia mayai mawili ama hugawanya yai lake lililorutubishwa na kusababisha watoto mapacha. Japokuwa kumekuwa na mabishano makali ambapo watu wengine wamekuwa na maoni hususani kwa upande wa mapacha wanaofanana kwa kusema kwamba mbegu ya kiume huwa na nguvu zaidi na hivyo kugawanya yai. Sina uhakika na jambo hilo ila kwa tafiti nyingi zilizofanywa na wanasayansi zinasema mwanamke ndiye mwenye uwezo wa kusababisha watoto mapacha yeye ama ndugu zake wa kike (wanaohusiana kibaiolojia).
Na hizi ni Sababu nyingine zinazoweza kuchangia watoto mapacha
1. Mwanamke anayetoka kwenye familia ambayo wanawake wana historia ya kupata mapacha.
2. Wanawake wenye asili ya kiafrika na kimarekani.
3. Wanawake wanaobeba mimba wakiwa na umri mkubwa, kuanzia miaka 35.
4. Wanawake wanene na wale warefu.
Kwa kuhitimisha
Kwa kifupi kama huna sababu zilizotajwa haina maana kwamba hauna uwezo wa kupata watoto mapacha. Uwezekano huo upo ila ni kwa kiwango kidogo kama wanawake wengine duniani. Kumbuka sababu zilizotajwa hapo juu hazihusiani na mapacha wanaofanana, inavyosemekana mwanamke yoyote ana uwezo wa kupata mapacha wanaofanana hata kama kwenye familia yake hakuna historia hiyo.
Nb
Maelezo yote yaliyotolewa hapa hayana maana kwamba ndiyo ukweli kwa asilimia mia moja la hasha kuna baadhi ya watu kwenye familia zao wanaamini kwamba watoto mapacha waliowapata wametokana na upande wa baba. Ila kwa asilimia kubwa inavyosemekana na wataalam wa masuala ya uzazi watoto mapacha husababishwa na mama pamoja na wanawake kutoka kwenye familia yake. Kama unataka kujifunza zaidi nakushauri soma zaidi tafiti mbalimbali.
JIUNGE NASI KWA KUTUFOLLOW

fb@edonetz  , twiter@edonetz  , inst@edonetz_blog  na  youtube@edone tv
 
Top