Sio kitu kibaya kujuliana hali na kutambulisha mambo ya msingi yanayoendelea katika mahusiano yako wewe na mpenzi wako kwa marafiki wa karibu au ndugu na jamaa kufahamu kushirikiana nanyi katika mapenzi yenu kama vile wakati wa sherehe au msiba.
Lakini kuna wakati watu wengine wa pembeni, wawe majirani, ndugu, wazazi au marafiki wanaweza kuwa wabaya au sumu ya mahusiano yako, hasa pale mnapotegemewa sana kutoa msaada, maoni au maelekezo katika maisha yako
Unaweza kufanya yafuatayo yatakusaidia sana.
Udhibiti wa taarifa kwa wengine: 
Kadri unavyoelezea mahusiano yako kwa watu wengine ndivyo unavyowapa nafasi watu kutoa maoni, na hata kudhani kuwa wana dhamana ya kukuelekeza unavyotakiwa kuishi na mwenza wako. Hivyo basi, chukua muda wa kutosha kutafakari na kufanya uchunguzi kuhusu masuala yako ya mahusiano kabla hajaanza kutafuta maoni, ushauri kwa watu wengine.
Upekee wa mambo:  
Tambua kuwa tabia ya mpenzi wako inaweza kuwa ni ya kipekee, mazingira pia ya tukio linalokufanya utake ushauri au maoni kwa wengine yanaweza kuwa ni ya kipekee, hivyo ushauri au maoni utakayopokea yanaweza yasikusaidie moja kwa moja katika suluhisho lako.
Mwenye maamuzi ni wewe: 
Ni kweli kuwa kuna nyakati ni muhimu kupata ushauri kutoka kwa watu wengine, na zaidi sana watu wenye uelewa sahihi na unaowaamini, hakikisha kuwa unatambua kuwa wewe mwenyewe ndio mwenye kubeba lawama ya maamuzi utakayochukua.
Kuwa na subira: 
Usichukue maamuzi ya haraka katika mahusiano hususani uamuzi wa kuamua kuwashirikisha watu wengine habari ya mambo yahusuyo uhusiano wako. Unapofanya uamuzi wa kuwashirikisha wengine kwa haraka  unajinyima nafasi ya kulichunguza jambo kwa ufasaha hususani madhara yanayoweza kutokea kwa kuwaeleza wengine, au kama ni tatizo, basi kufikiria njia sahihi ambazo ungeweza  kuzitumia kupata suluhu ya tatizo.
Fungua njia za mawasiliano kati yenu: 
Pengine chanzo cha wewe kutaka kuzungumza mambo ya ndani yanayohusu mahusiano yenu kwa watu wengine ni kwa kuwa umekosa  nafasi ya kuzungumza kwa ufasaha na mwenzi wako. Tafuteni nafasi za kutosha, jengeni mazingira ya kuzungumzia mambo yenu kabla ya kutaka kuwashirikisha watu wengine.
Kuweni peke yenu:
Hata kama hautaki kueleza watu kuhusu mambo yanayoendana na maisha yenu, mazingira unamoishi yanaweza kuchangia watu kutaka kuingilia mahusiano yenu kwa kutoa maelekezo, ushauri au maoni kuhusu muishivyo wewe na mpenzi wako. Inapobidi hakikisha hamuishi karibu na wazazi wenu, ndugu au rafiki wa karibu.
Jifunze zaidi :

Kumbuka mahusiano yanahitaji sana uelewa mkubwa wa jinsi ya kufanya mawasiliano fasaha, kuelewa hisia za mwenzi wako, kutambua mbinu za kusuluhisha migogoro na zaidi sana kufanya mipango ya muda mrefu ya uhusiano wenu. Jizoeshe kusoma makala na vitabu mbalimbali vyenye kuboresha ufahamu wa mambo ya msingi. 
JIUNGE NASI KWA KUTUFOLLOW
fb@edonetz  , twiter@edonetz  , inst@edonetz_blog  na  youtube@edone tv
 
Top