Kuacha kazi kunaweza kuwa ni jambo zuri katika maisha yako. Ukweli ni kuwa ni vigumu kupata kazi uipendayo kwa asilimia 100.
Hata hivyo, kama unapenda kuwa na kazi ambayo inatimiza matakwa yako, kwa hakika hutokubali kufanya kazi usiyoipenda. Na hata kama upo kwenye kazi unayoipenda, kuna matatizo ambayo ukikutana nayo ni ishara kwamba umefikia muda wa kusonga mbele kwingine.
Zifuatazo ni dalili 10 zinazokuonyesha kwamba umefikia muda wa kuacha kazi unayofanya sasa.
Ujuzi wako hautumiki ipasavyo
Watu wengi wenye motisha huanza kutoridhika kama wanatumia muda wao mwingi kwenye kazi ambayo haitumii ujuzi wao ipasavyo. Kama wewe ni mmoja wa watu hawa ni bora ukatumia muda wako kutafuta kazi ambayo itatumia ujuzi wako ipasavyo.
Unafanyishwa kazi kupita kiasi bila kulipwa fidia
Waajiri wengi Tanzania hawalipi wafanyakazi wao wanapofanya kazi ndani ya muda wa nyongeza.
Ingawa kila kazi ina wakati ambao wafanyakazi wanatakiwa kufanya kazi nje ya muda wa kazi, hautakiwi kufanya hivyo mara kwa mara kwani itakusababishia kuwa mchovu na kushindwa kufanya kazi vizuri.
Umechoka na huna motisha
Hutokea wakati mwingine kazi au kampuni inakua sio sahihi kwako. Aidha, huamini ujumbe au maadili ya kampuni au huridhishwi na kazi unayofanya. Hii ni dalili kuwa hapo hapakustahili kwa sasa.
Humheshimu au kumuamini bosi wako
Moja ya sababu kubwa za watu kuacha kazi ni kumchukia bosi wao, na hili ni kweli hasa kama bosi huyo anafanya haya: anachukua sifa kwa kazi uliyofanya wewe bila kukiri mchango wako, haangalii maslahi yako anapofanya makubaliano ya kazi na mabosi wake, anajifanya kukusikiliza lakini hafanyii kazi maoni au malalamiko yako au hakuheshimu.
Ujuzi wako umezidi kazi unayofanya
Wakati mwingine unakuta umejifunza vyote ambavyo unaweza kujifunza kutoka kwenye nafasi uliyopo, hivyo hupati changamoto zozote. Kama hakuna nafasi ya kuhamia sehemu nyingine kwenye kampuni hiyohiyo basi ni muda wa kuhama kampuni.
Hupendi utamaduni wa kampuni
Ni muhimu kupenda mazingira yako ya kazi. Kwa mfano, baadhi ya ofisi zinaweza kuwa na kelele mno au kuwa na sheria kali. Mwenyewe unajijua vizuri na unajua ni mazingira gani yatakufaa zaidi.
Unalipwa chini ya kiwango
Pesa haitakiwi kuwa sababu kuu ya wewe kufanya kazi ufanyayo. Lakini kazi yako inatakiwa ikuwezeshe kumudu gharama za msingi za maisha hasa kama unaishi maeneo ya miji mikuu ambayo maisha yako juu.
Kampuni yako haiwekezi kwako
Ni muhimu kwenda na wakati kwa kujua yanayojiri katika sekta yako ili uongeze uwezo wako wa kufanya kazi. Lakini kama kampuni yako haiko tayari kulipia kozi zitakazokusaidia kuongeza ujuzi wako kazini, hii ni dalili kwamba hawakuthamini. Tafuta sehemu nyingine.
Unahisi kwamba hii ni ‘kwa ajili ya sasa’
Kama unahisi ajira yako ni ya muda na haikufai kwa muda mrefu, ni bora uache hasa kama ni kazi usiyoitaka.
Umepata ofa nzuri kwingine
Kama umepata ofa ya kazi ambayo itakufaa zaidi, Hiyo ni sababu rahisi ya kukufanya uache kazi uliyo nayo sasa.
Kumbuka
Watu wengi hutafuta kazi nyingine pale tu wanapoacha kazi au kwa kutoridhishwa na kazi walizonazo, hili lina hasara kwako kwa sababu itasababisha kukubali kazi isiyo kufaa.
Muda wote tafuta kazi, hii itakuonyesha nafasi zilizopo na utakapopata ofa au kuitwa kwenye mahojiano itakujulisha thamani yako kwenye soko la ajira.


JIUNGE NASI KWA KUTUFOLLOW
fb@edonetz  , twiter@edonetz  , inst@edonetz_blog  na  youtube@edone tv
 
Top